Saturday 9 July 2016

#YALIYOJIRI>>>>WAPATA KIPINDUPINDU WAKIWA IBADANI.Fahamu zaidi hapa.

WAUMINI zaidi ya 300 kutoka mikoa mbalimbali nchini waliokuwa wameweka kambi kwa ajili ya kushiriki kongamano la Kanisa la Sauti ya Uponyaji la Nabii Joshua, eneo la Kihonda- Veta, Manispaa ya Morogoro wamelazimika kurejea makwao kutokana na kongamano hilo kusitishwa, baada ya baadhi yao kuugua ugonjwa wa kipindupundu na kulazwa kambi maalumu ya Kituo cha Afya cha Sabasaba cha mjini Morogoro.

Ofisa Afya wa Manispaa ya Morogoro, Gabriel Malisa,  alieleza kuhusu baadhi ya waumini wa kanisa hilo kupata ugonjwa wa kipundupindu walipokuwa wamekusanyika na kukesha katika kambi ya kanisa hilo kwa ajili ya maombezi kutoka kwa nabii huyo.

Malisa alisema kongamano hilo lilianza Julai 6, mwaka huu eneo la mtaa wa Wespa, Kata ya Kihonda, Manispaa ya Morogoro liliko kanisa hilo na waumini wakiwa katika mkesha wa maombi, baadhi yao walikumbwa na ugonjwa wa kipindupindu na kufikishwa Kituo cha Afya Sabasaba kupatiwa matibabu na kulazwa.

“Tulipopata taarifa ya wagonjwa wawili wa kipindupindu wanaofikishwa kutibiwa kituo cha Afya cha Sabasaba na walitokea kwenye kongamano hilo, timu ya wataalamu wa afya ililazimika kufika eneo hilo na kubaini kuwepo mazingira hatarishi, tulichukua uamuzi kuwa kongamano lisitishwe na kuwataka waondoke,” alisema.

Malisa alisema walimtaka Nabii Joshua kusitisha kongamano hilo na waumini waliotoka mikoa mbalimbali ikiwemo ya Kigoma na Dodoma waliamriwa warejee makwao. Alisema uamuzi huo ulichukuliwa baada ya idadi ya wagonjwa kuzidi kuongezeka na kufikia saba wakiwa wamelazwa katika kambi ya wagonjwa wa kipindupindu, Kituo cha Afya Sabasaba kwa ajili ya matibabu.

“Timu ya wataalamu wa afya ilitembelea tena eneo hilo Julai 7, mwaka huu na ilikuta kongamano hilo limehamishwa katika ukumbi wa nyumba ya kulala wageni ya Magunila,” alisema.

Alisema baada ya kubaini jambo hilo, serikali ya wilaya ya Morogoro pamoja na Uongozi wa Manispaa ulimwamuru Nabii Joshua kulifunga kongamano hilo na waumini wake warudi makwao baada ya kuonekana idadi ya wagonjwa kutoka kwenye kongamano hilo kuendelea kuongezeka.

0 comments:

Post a Comment