Home »
Habari Moto
» #YALIYOJIRI>>>>WAPATA KIPINDUPINDU WAKIWA IBADANI.Fahamu zaidi hapa.
WAUMINI zaidi ya 300 kutoka mikoa
mbalimbali nchini waliokuwa wameweka kambi kwa ajili ya kushiriki
kongamano la Kanisa la Sauti ya Uponyaji la Nabii Joshua, eneo la
Kihonda- Veta, Manispaa ya Morogoro wamelazimika kurejea makwao kutokana
na kongamano hilo kusitishwa, baada ya baadhi yao kuugua ugonjwa wa
kipindupundu na kulazwa kambi maalumu ya Kituo cha Afya cha Sabasaba cha
mjini Morogoro.
Ofisa Afya wa Manispaa ya Morogoro,
Gabriel Malisa, alieleza kuhusu baadhi ya waumini wa kanisa hilo kupata
ugonjwa wa kipundupindu walipokuwa wamekusanyika na kukesha katika
kambi ya kanisa hilo kwa ajili ya maombezi kutoka kwa nabii huyo.
Malisa alisema kongamano hilo lilianza
Julai 6, mwaka huu eneo la mtaa wa Wespa, Kata ya Kihonda, Manispaa ya
Morogoro liliko kanisa hilo na waumini wakiwa katika mkesha wa maombi,
baadhi yao walikumbwa na ugonjwa wa kipindupindu na kufikishwa Kituo cha
Afya Sabasaba kupatiwa matibabu na kulazwa.
“Tulipopata taarifa ya wagonjwa wawili
wa kipindupindu wanaofikishwa kutibiwa kituo cha Afya cha Sabasaba na
walitokea kwenye kongamano hilo, timu ya wataalamu wa afya ililazimika
kufika eneo hilo na kubaini kuwepo mazingira hatarishi, tulichukua
uamuzi kuwa kongamano lisitishwe na kuwataka waondoke,” alisema.
Malisa alisema walimtaka Nabii Joshua
kusitisha kongamano hilo na waumini waliotoka mikoa mbalimbali ikiwemo
ya Kigoma na Dodoma waliamriwa warejee makwao. Alisema uamuzi huo
ulichukuliwa baada ya idadi ya wagonjwa kuzidi kuongezeka na kufikia
saba wakiwa wamelazwa katika kambi ya wagonjwa wa kipindupindu, Kituo
cha Afya Sabasaba kwa ajili ya matibabu.
“Timu ya wataalamu wa afya ilitembelea
tena eneo hilo Julai 7, mwaka huu na ilikuta kongamano hilo limehamishwa
katika ukumbi wa nyumba ya kulala wageni ya Magunila,” alisema.
Alisema baada ya kubaini jambo hilo,
serikali ya wilaya ya Morogoro pamoja na Uongozi wa Manispaa ulimwamuru
Nabii Joshua kulifunga kongamano hilo na waumini wake warudi makwao
baada ya kuonekana idadi ya wagonjwa kutoka kwenye kongamano hilo
kuendelea kuongezeka.
0 comments:
Post a Comment