WAZIRI
 wa Fedha na Mipango, Dk Phillip Mpango amesema hatua ya Serikali ya 
kukusanya kodi kwa nguvu kwa baadhi ya wafanyabiashara waliotorosha 
makontena bila kulipiwa ushuru, haikuwa lengo la kumkomoa mtu, bali 
ililenga kukusanya fedha za Serikali yenye lengo la kuifanya nchi iache 
utegemezi wa wahisani.
Waziri
 huyo ambaye jana alikutana na makundi mbalimbali ya wafanyabiashara 
ofisini kwake Dar es Salaam, alisema yeye kama waziri wa fedha 
asingependa kuwa waziri ombaomba kwa wahisani, ambao alidai baadhi yao 
wana masharti magumu, ambayo hayatekelezeki kwa maadili ya Watanzania.
“Nimewasindikiza
 wenzangu huko nje kuomba fedha sasa nimechoka, nataka kutembea kifua 
mbele, maana wana masharti magumu, wengine wanataka turuhusu homosexual 
(ndoa za jinsia moja), masharti haya kwa kweli yanakera sana,” alisema Dk Mpango ambaye katika serikali iliyopita alikuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango.
Dk
 Mpango aliongeza kuwa ili nchi isonge mbele, ni lazima ikusanye kodi ya
 kutosha; na jana aliahidi kuchukua hatua kadhaa, zitakazoiwezesha sekta
 binafsi kuwa mhimili wa kuimarisha uchumi wa nchi ili kufikia malengo 
ya kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye kipato cha kati.
Alisema
 Rais John Magufuli ni kiongozi ambaye akilala na kuamka, anawaza namna 
ambavyo atawahudumia wananchi wake, ambao wengi wako kwenye dimbwi la 
umaskini. 
Alisema Rais atafanikiwa tu, pale Serikali yake itakusanya kodi ya kutosha na kuwahudumia wananchi hao.
“Kuna
 minong’ono kwamba eti Serikali ya Awamu ya Tano inawanyanyasa 
wafanyabiashara wakubwa na kwamba hatua tulizochukua kukusanya kodi, 
ililenga kuwadhalilisha baadhi ya wafanyabiashara, hii sio kweli 
kabisa,” alisema Dk Mpango.
Dk
 Mpango alisema Serikali ya Awamu ya Tano, inatambua umuhimu wa 
wafanyabiashara, hivyo wizara yake itakuwa ya mwisho kuchukua hatua za 
kuwanyanyasa. 
“Nawahakikishia
 kwamba nina dhamira ya dhati ya kufanya kazi kwa kushirikiana na ninyi 
wafanyabiashara wakubwa na wadogo ili tutimize ndoto ya Rais,” alisema.
Alisema
 serikali yoyote duniani ni lazima ikusanye kodi, hivyo aliwahakikishia 
wafanyabiashara hao kuwa kama bado kuna wafanyabiashara wanaokwepa au 
hawataki kulipa kodi kwa mujibu wa sheria, serikali haitakuwa tayari 
kuwavumilia.
Dk
 Mpango alisema idadi ya watu wanaolipa kodi kwa sasa nchini bado 
wachache, hivyo aliwaagiza wafanyabiashara wote kujisajili wapatiwe 
Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN).
Pia,
 aliwataka waache tabia ya kufanya udanganyifu kwa kuwa na vitabu vingi 
vya utunzaji wa kumbukumbu za biashara. Aliwaagiza kuhakikisha wanatoa 
stakabadhi na suala hilo lisiwe hiyari.
“Tunajua kwamba mnatoa vitisho kwa wanunuzi kuwa kama wanataka risiti bei ni ya juu, hiki mnachofanya ni hatari kwa nchi,” alisema na kuwataka wote watumie mashine za EFD na serikali inaendelea na mpango wa kununua zingine ili wagawiwe bure.
Aliwataka
 kutoa taarifa kwa Kamishna Mkuu wa TRA, kama kuna mfanyakazi wa Mamlaka
 ya Mapato (TRA) au wa Halmashauri ya Wilaya, ambaye atadai hongo au 
atawanyanyasa wakati wa kudai kodi.
Katika kutekeleza hilo, aliwapatia namba zake pamoja na za Kamishna na kuwataka waache tabia ya kutoa rushwa ili wasilipe kodi.
 Dk
 Mpango alisema baada ya wafanyabiashara kufanya kikao na Rais Magufuli,
 Serikali imeunda kikosi kazi kushughulikia kero zote, zilizotolewa na 
Baraza la Biashara na mojawapo ni kufuta utiriri wa kodi ili kuwapa 
wepesi wawekezaji kufanya biashara nchini na kumpungumzia mzigo mkulima.
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment