Maalim Seif Sharif Hamad
Vyama tisa vya siasa kati ya 14 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu Zanzibar 
mwaka jana vimeungana na CUF kutoshiriki uchaguzi wa marudio uliopangwa 
kufanyika Machi 20, hadi utakapopatikana mwafaka wa kumaliza mgogoro wa 
kisiasa. 
Mratibu wa umoja wa vyama hivyo, Kassim Bakari Ali 
alisema jana kuwa vyama hivyo vilikutana Unguja na 
kupitisha maazimio mawili ya kutoshiriki uchaguzi huo. 
Vyama hivyo ni 
UMD, Jahazi Asilia, Chaumma, UPDP, DP, CCK na ACT Wazalendo. Ushiriki wa 
vyama vya ADC na CCK bado una utata kutokana na wagombea wake kutangaza 
kushiriki licha ya vyama vyao kuwa na msimamo tofauti, hali 
iliyosababisha wagombea hao kusimamishwa. 
Vyama ambavyo 
vimetangaza kushiriki marudio hayo hadi sasa ni CCM, Tadea, TLP, Sau na 
AFP. 
Kwa kipindi cha miezi miwili iliyopita, Zanzibar imeendelea kuwa 
kwenye mgogoro wa kisiasa kati ya vyama vikubwa vinavyounda Serikali ya 
Umoja wa Kitaifa (SUK) baada ya CUF kususia marudio ya uchaguzi baada ya
 ule wa awali kufutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), 
Jecha Salim Jecha. 
Akitaja maazimio ya vyama hivyo, Kassim 
alisema wamekubaliana kutoshiriki marudio ya uchaguzi huo hadi mgogoro 
wa CCM na CUF utakapomalizika na wameunda kamati ya wajumbe 18 ya 
wenyeviti na makatibu wa kila chama ili kuanzisha meza ya kutafuta 
suluhu ya mvutano uliopo kati ya CCM na CUF.
 “Tutaanza kukaa na viongozi
 wa vyama hivyo kila upande kujua ni nini hasa hatima ya mvutano huo na 
tunajikwamuaje,” alisema. 
Ali ambaye pia ni mwenyekiti wa Jahazi
 Asilia alisema mgogoro wa Zanzibar utamalizwa na Wazanzibari wenyewe, 
hivyo ni vyema viongozi hao wa kisiasa wakajenga uvumilivu katika 
kutafuta mwafaka. 
Alisema tatizo la vyama hivyo siyo kushiriki 
marudio ya uchaguzi huo tu bali ni kuangalia chanzo na hatima ya mgogoro
 huo kwa masilahi ya Wazanzibari. 
Mwenyekiti 
wa CCK, Constatine Akitanda aliwaambia waandishi wa habari kuwa uamuzi 
wa kusimamishwa uanachama kwa mgombea wake wa urais, Ali Khatibu Ali, 
unakwenda sanjari na kutoshiriki uchaguzi hadi maridhiano ya CUF na CCM 
yapatikane. 
Mgombea urais wa Zanzibar kupitia AFP, Said Soud 
Said alisema jana kwamba, chama hicho kimekubali kurudia uchaguzi huo.
 “Lengo la chama chetu ni kushika dola, sasa tusiposhiriki itakuwaje? 
Kwanza hatuamini kama CUF haijatendewa haki kwa sababu ni kweli kulikuwa
 na udhaifu, mfano vurugu za kituo cha kupigia kura cha Matrekta Wawi,” alisema. 
Mwenyekiti
 wa TLP, Augustine Mrema alisema kama vyama hivyo viliiamini ZEC katika 
uchaguzi uliopita, vinatakiwa kuiamini kwenye marudio hayo kwa kuwa 
hakuna mbadala.
“Naomba wakubali kurudia uchaguzi kwani ‘maji 
yalishamwagika na kuzoleka haiwezekani... Nani aliyekwenda mahakamani 
kupinga? Wanachoogopa kurudia ni kitu gani kama walishinda?” alihoji Mrema.
 
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment