Nimetoka Kituo Kikuu cha Polisi Dar sasa hivi. Polisi wamekataa 
kunirudishia simu yangu waliyoinyang'anya kwa nguvu tarehe 6 Machi, siku
 waliyonikamata nikiwa mahakamani Kisutu.
Mimi sijatuhumiwa wala kushtakiwa kwa kosa lolote la mtandao chini ya 
Sheria ya Makosa ya Mtandao au Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na
 Kiposta.
Badala yake nimeshtakiwa kwa makosa ya uchochezi yanayohusiana na kauli 
zangu juu ya Serikali ya Rais Magufuli. Aidha, nimeshtakiwa kutokana na 
msimamo wangu na kauli zangu juu ya siasa za Zanzibar na masuala ya 
Muungano.
Kwa sababu hizi, Jeshi la Polisi halikuwa na, na halina, sababu wala 
haki ya kuchukua simu yangu na kuendelea kukaa nayo hadi sasa, siku 17 
baadae.
Nimepata taarifa kwamba tangu walipoichukua kwa nguvu karibu wiki tatu 
zilizopita, simu hiyo imekuwa inaonekana inatumika kwa mawasiliano ya 
whatsapp.
Maana yake ni kwamba polisi wanasoma na au kusikiliza mawasiliano yangu 
ya simu na ya kielektroniki. Hii ni kinyume cha sheria za nchi yetu.
Simu hiyo ni chombo changu cha mawasiliano ya kikazi na binafsi. Kama 
mbunge, ninaitumia simu hiyo kwa ajili ya mawasiliano yangu na wananchi 
walionichagua na viongozi wengine wa kiserikali na kichama.
Jeshi la Polisi halina haki ya kujua au kuingilia mawasiliano hayo.
Kama wakili ninatumia simu hiyo kwa ajili ya mawasiliano na wateja 
wangu, wengi wao wakiwa na kesi mahakamani dhidi ya Jeshi la Polisi au 
Serikali hii.
Mawasiliano hayo yanalindwa kwa mujibu wa sheria na polisi hawana sababu
 wala haki ya kujua au kuingilia mawasiliano hayo na wateja wangu.
Vile vile ninatumia simu yangu kwa mawasiliano yangu binafsi na familia yangu, marafiki zangu na jamaa zangu wengine.
Mawasiliano haya nayo yanalindwa na Katiba yetu na polisi hawana sababu 
wala haki ya kujua au kuingilia mawasiliano hayo binafsi.
Kwa vyovyote vile, kitendo cha Jeshi la Polisi kuchukua na kuendelea 
kuishikilia simu yangu bila sababu wala haki ni mfano mwingine wa 
matumizi mabaya ya mamlaka ya kiupelelezi ya Jeshi hili la Polisi.
Badala ya kushughulikia wahalifu wa wazi kama akina Daudi Bashite na 
wenzake, polisi wetu wanahangaika na viongozi waliochaguliwa na wananchi
 wanaotumia haki na wajibu wao kikatiba kuikosoa serikali ya Rais 
Magufuli kwa sababu ya matendo yake ya hovyo.
Ninafahamu polisi wanafikiri kwamba kwa kunifanyia vitendo hivi basi 
nitaogopa na kulegeza msimamo wangu katika masuala mbali mbali 
yanayolisibu taifa letu.
Ninawaomba wajiulize kwa nini imeshindikana hadi sasa kulegeza msimamo 
wangu huo kwenye masuala hayo, licha ya kunikamata na kuninyanyasa mara 
nyingi kwenye vituo vya polisi na mahakamani. Sitishiki na sitatishika 
na mambo yao haya.
Hata hivyo, naomba niseme wazi ili mwenye kusikia na asikie. Vitendo 
hivi vya Jeshi la Polisi havifai na vinatakiwa kukoma kabisa. Polisi 
wanirudishie simu yangu mara moja na bila masharti yoyote.
Ninaendelea kutafuta mawasiliano ya IGP Mangu na wakubwa wenzake ili wanieleze kwa nini simu yangu inashikiliwa na maofisa wao.
Endapo na wao watashindwa kutoa maelekezo sahihi kwa waliochukua simu 
yangu na wanaendelea kukaa nayo, nitalazimika kwenda Mahakama Kuu ili 
kuomba mahakama iingilie kati na kutamka kama ni sahihi kisheria kwa 
mapolisi wa nchi hii kuingilia mawasiliano ya sisi wananchi kwa namna ya
 hovyo namna hii.
Naomba mnaopata ujumbe huu mnisaidie kupaza sauti zetu ili matendo haya mabaya yakome katika nchi yetu.
Wasalaam,
Mh. Tundu AM Lissu
Download Application ya Hebron Malele Blog Kwenye Simu yako Kusoma Habari Zetu Kwa Urahisi>>>>Bonyeza Hapa
Follow me instagram>>>Bonyeza Hapa













0 comments:
Post a Comment