MBUNGE wa Nzega Mjini, Hussein Bashe (CCM), amedai kupewa taarifa na 
mawaziri kuwa muda wowote anaweza kuuawa na kikundi maalumu 
kinachoendesha utekaji nchini.
Aidha, Bashe amedai kuwa mbali na yeye kuwa katika hatari hiyo, pia 
ameambiwa na mawaziri hao wa serikali kuwa kuna wabunge wengine 10 ambao
 wanawindwa na kikundi hicho na wametahadharishwa 'kuwa makini 
barabarani'.
Bashe (41), aliyasema hayo bungeni mjini hapa jana asubuhi aliposimama 
na kukiomba Kiti cha Spika kuahirisha shughuli za Bunge ili kujadili 
hoja ya dharura akitumia Kanuni ya 47(1),(2)na (3) vya Kanuni za Kudumu 
za Bunge toleo la Januari 2016.
Huku akiungwa mkono na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (Chadema) 
na kushangiliwa na baadhi ya wabunge, Bashe alisema kumekuwa kukitokea 
matukio ya sintofahamu yanayowahusu wabunge na raia wa kawaida 
yanayoendeshwa na kikundi hicho ambacho alidai kinatoka idara nyeti 
serikalini.
Katika kujenga hoja yake, Bashe alisema Mbunge wa Geita, Joseph Kasheku 
(CCM), mbunge wa zamani Mkuranga mkoani Pwani, Adam Malima (CCM), msanii
 Roma Mkatoliki na yeye mwenyewe ni miongoni mwa watu waliowahi kutekwa 
huku akikumbushia pia madai ya kupotea kwa Ben Saanane ambaye ni 
msaidizi wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.
Aliliomba shughuli za Bunge ziahirishwe ili wabunge wajadili jambo la 
dharura ambalo limekuwa likitokea kwa muda mrefu katika nchini.
"Miongoni mwa watu waliowahi kutekwa ni Mheshimiwa Musukuma (Joseph 
Kasheku), Mheshimiwa Bashe kwenye mkutano mkuu wa CCM, ndugu Malima, Ben
 Saanane amepotea... (makofi), juzi amepotea Roma Mkatoliki," alisema 
Bashe huku akishangiliwa na baadhi ya wabunge kwa kugonga meza.
Alisema zaidi: "Nasema ni jambo la dharura kwa sababu hawa ni wale ambao
 wanafahamika. Hatujui Watanzania wangapi hawafahamiki katika ngazi za 
chini.
"Na zipo taarifa ambazo binafsi nimezipokea kutoka kwa baadhi ya 
mawaziri, wakinitahadharisha mimi binafsi kwamba 'Bashe kuwa makini, 
wewe ni mmoja kati ya wabunge 11 ambao wamewekwa katika 'list' (orodha).
 Mkikaa barabarani vibaya, mnaweza kupoteza maisha yenu'.
"Nasema jambo hili ni dharura kwa sababu kikundi hiki kilichomo ndani ya
 idara ya ... (alitaja idara nyeti), ambacho kimeamua kuchukua mamlaka 
haya ya kuteka watu, kinaharibu heshima ya serikali yetu, kinaharibu 
heshima ya chama changu ambacho mimi na wabunge wenzangu wa CCM, 
tuliomba ridhaa ya kutaka kuwaongoza Watanzania na siyo kuwahatarishia 
maisha yao."
Bashe alimuomba Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, kuruhusu jambo 
hilo lijadiliwe na wabunge na ikiwezekana chombo hicho cha kutunga 
sheria kiunde kamati maalumu ya kuchunguza jambo hilo.
Bashe pia alimuomba Naibu Spika kutumia mamlaka yake kuiagiza Kamati ya 
Kudumu ya Bunge ya Usalama na Mambo ya Nje kufanya kazi changamoto hiyo 
na kulipatia Bunge taarifa kwa ajili ya usalama wa nchi.
"Hali ya nchi siyo salama, Watanzania wana taharuki, Watanzania 
wanajadili mambo haya katika mitandao na 'there is no statement' (hakuna
 kauli) toka serikali.
Waziri wa Mambo ya Ndani..." Bashe alisema huku akikatishwa na Naibu 
Spika ambaye alimtaka aketi ili Kiti cha Spika kiangalie Kanuni ya 47 
inaeleza nini kuhusu madai yake.
Kabla ya kutoa uamuzi wa Kiti kuhusu madai ya Bashe, Naibu Spika alitoa 
nafasi kwa Sugu kueleza hoja yake bungeni baada ya mbunge huyo kusimama 
na kuomba kupewa nafasi ya kuwasilisha hoja ya dharura bungeni.
Akitumia Kanuni ya 47, Sugu aliunga mkono hoja ya Bashe kwamba Bunge 
liahirishe shughuli zake za jana na kujadili hoja ya dharura ya kadhia 
ya utekaji na kupotea kitatanishi kwa watu nchini.
"Taifa limekuwa gizani kwa utamaduni mpya uliozuka wa kuteka watu, 
utamaduni ambao si wa kwetu, ni utamaduni wa kimafia, utamaduni ambao 
kwa mara ya mwisho kwenye mipaka ya Bara na visiwani, tuliusikia 
alipotekwa Mzee Kassim Hanga kule Zanzibar miaka hiyo," Sugu alisema.
"Lakini tangu kipindi hicho haujakuwapo tena. Toka operesheni hii ya 
kuteka watu nyara ianze, kila anayehusika na usalama likiwamo Jeshi la 
Polisi, 'always' (mara kwa mara) wanasema 'hatujui, hatujawaona kwenye 
vituo vyote'.
Nchi inabaki kwenye tahayari, kapotea Ben Saanane, mara miili sita, saba
 imeopolewa kwenye Mto Ruvu ikaenda kuzikwa bila kufanyiwa 'post-mortem'
 (uchunguzi) kwa amri ya ambaye hatujui ni nani.
"Bashe alitekwa, Nape (Nnauye) alitekwa, akaokolewa na Maulid Kitenge, 
vinginevyo pengine angekuwa ametekwa, hakuna mtu aliyezungumza kitu."
Kutokana na changamoto hiyo mpya nchini, Sugu alimshauri Waziri wa Mambo
 ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, kuachia ngazi ili kulinda heshima 
yake kama kweli bado ana matumaini ya kuwa Rais wa Tanzania.
"Waziri wa Mambo ya Ndani yuko kimya mpaka najiuliza kama anabanwa kiasi
 hicho, huyu ni mtu 'potential' (muhimu) ambaye alifikia hatua ya 
kugombea urais na bado ana 'future'," Sugu alisema.
"Kwanini asijiuzulu, akalinda heshima yake kuliko kukaa kwenye 'mess' (aibu)? Alihoji Sugu. "Kujiuzulu ni utamaduni mzuri.
Mzee (Alhaji Ali Hassan) Mwinyi alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani miaka 
hiyo, mwaka '76, ikatokea messy (kuboronga), 'aka-bounce back' 
(akarejea), miaka ya '80 akaja kuwa Rais wa nchi hii.
"Ndugu yangu Mwigulu, nikushauri kama hushirikishwi, mambo yanafanyika, hamna mtu anakuja na majibu.
"Lakini juzi baada ya kutekwa Roma Mkatoliki, tumepata mwanga. Yupo mtu 
Dar es Salaam alituambia anajua Roma aliko na angerudi kabla ya 
Jumapili.
"Kama Waziri Kivuli (wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo), nikatoka 
Jumamosi na 'ku-demand' (kuagiza) kwamba aachiwe siku ileile na 
akaachiwa, nashukuru Mungu. Sasa basi, hatujui nani 'next' (anayefuata) 
atatekwa. Yawezekana Sugu ingawa mimi 'I don't care much' (sijali) kwa 
sababu Mbeya wataziba nafasi yangu.
"Lakini Naibu Spika 'it could be you' (yaweza kuwa wewe). 'It is the 
war' (ni vita), 'no body is safe' (hakuna aliye salama. Kwanini Bunge 
hili lisijadili na hatimaye limlazimishe Bashite kama alivyojua kwamba 
Roma Mkatoliki yuko wapi na angemrudisha Jumapili, tumlazimishe sasa 
Bunge hili tujadili na baadaye tumlazimishe Bashite atutajie aliko Ben 
Saanane na atutajie kwamba ili miili iliyotupwa Ruvu na kuzikwa haraka 
haraka bila kufanyiwa 'post-mortem' ni ya kina nani kwa sababu huyu 
anaonekana anajua undani wa mambo haya."
KULIPATIA UFUMBUZI
Akijibu maombi ya wabunge hao, Naibu Spika alikataa kuruhusu jambo hilo 
kujadiliwa bungeni kwa kupitia utaratibu wa hoja ya dharura kwa kuwa 
vyombo vya sheria vinaweza kulipatia ufumbuzi.
Dk. Acskon alisema jambo la dharura linaloweza kusababisha kuahirishwa 
kwa shughuli za Bunge kulijadili ni lile lenye maslahi kwa umma na iwapo
 utatuzi wake unategemea zaidi ya utekelezaji wa kawaida wa sheria.
"Waheshimiwa Bashe na Sugu wameeleza kwa kirefu kuhusu jambo ambalo 
limetokea hapa na pale, lakini pia tumeliona kwenye vyombo vya habari na
 tumelisoma," Dk. Ackson alisema.
"Maelezo yao kwa ujumla yanahusu mambo ambayo yanawapata wananchi ambayo
 watu kadhaa wametajwa kama mifano kwamba wamekuwa wakitekwa ama 
wamekuwa wakikamatwa.
"Sasa, nadhani wote tunafahamu matakwa ya Kanuni ya 47, hili jambo la 
hawa watu kukamatwa ama kutekwa kwa sababu sasa hata wale waliokamatwa, 
na wao wamewekwa kwenye kundi la kutekwa. Sasa sijui kama tunaweza 
kuyatenganisha haya mambo mawili; nani amekamatwa na nani ametekwa?
"Lakini maelekezo yaliyotolewa kwa kirefu ni kwamba wakati mwingine mtu 
akiwa haonekani, polisi ndiyo sehemu ya kwanza ambayo inaulizwa na yapo 
mazingira polisi haijatoa maelezo kwamba hawa watu wako wapi na mifano 
imekwishatajwa.
"Mheshimiwa Bashe amekwenda mbali zaidi akisema kwamba kipo kikundi ambacho kinafanya kazi hiyo.
Na Mheshimiwa Joseph Mbilinyi na yeye ameeleza kwamba hili jambo sasa 
limekuwa kama utamaduni kwa maana ya kwamba linatokea kila wakati na 
akaenda mbele zaidi na kumshauri Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya 
Nchi (Nchemba) kwamba aweze kujiuzulu akiona inafaa.
"Kanuni ya 47 huwa ni lazima isomwe pamoja na (Kanuni ya) 48 kwa sababu 48 ndiyo inayoweka masharti ya matumizi ya Kanuni ya 47.
Sasa kwa kuwa Kanuni ya 48(4) nitaisoma, inasema hivi 'jambo lolote 
litahesabiwa kuwa ni lenye maslahi kwa umma iwapo utatuzi wake 
unategemea kuwa zaidi kuliko zile za utekelezaji wa kawaida wa sheria 
peke yake.
"Masuala haya yaliyoulizwa na Mheshimiwa Bashe na pia yaliyoulizwa na 
Mheshimiwa Mbilinyi yako chini ya utaratibu wa kisheria na Bunge hili 
litashughulika na mambo ambayo ni yenye maslahi ambayo sheria haina 
uwezo wa kuyatolea majibu.
Kwa sababu hiyo, sitalihesabu hili jambo kwa mujibu wa Kanuni ya 47(4) 
kwamba ni jambo la dharura lakini ni jambo ambalo utaratibu wa kawaida 
wa kisheria unaweza ukafanya kazi. Hayo ndiyo majibu yangu kuhusu 
matumizi ya Kanuni ya 47.
Matukio ya kupotea, kutekwa na kuuawa kwa wanasiasa nchini ni nadra, 
ingawa Juni 12, mwaka jana, chama cha ACt-Wazalendo kilidai kiongozi 
wake mkuu, Zitto Kabwe, alikuwa hajulikani alipo kwa zaidi ya saa 12 
huku akiwa anasakwa na Jeshi la Polisi.
Download Application ya Hebron Malele Blog Kwenye Simu yako Kusoma Habari Zetu Kwa Urahisi>>>>Bonyeza Hapa
Follow me instagram>>>Bonyeza Hapa
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment