Saturday 28 November 2015

#YALIYOJIRI>>>"Dili Limebumbulika"Magogo ya Milioni 300 Yakamatwa Bandarini Yakipelekwa Nchini China Kinyemela.Fahamu zaidi hapo.

Kontena 37 zenye shehena ya magogo aina ya mninga yenye thamani zaidi ya Sh. milioni 300 zimekamatwa zikiwa zinasafirishwa kuelekea nchini China bila kibali.
Katika shehena hiyo, kontena 31 zimekamatiwa katika Bandari ya Dar es Salaam, kati ya hizo mbili zimekamatwa mkoani Mbeya,  na mikoa ya Rukwa na Pwani katika maeneo ya Kibaha na Kongowe, kontena moja kila sehemu na Mbezi ya jijini Dar es Salaam, pia imekamatwa kontena moja na kufanya idadi ya kontena zilizokamatwa kufikia idadi 37.

Kontena hizo zinazodaiwa kutoka nchini Zambia, zimekutwa hazina kibali cha usafirishwaji na kusababisha serikali kupoteza mamilioni ya fedha. 
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam jana,  Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Adelhelm Meru, alisema kontena hizo zimeonyesha kupitishwa mpaka wa Tunduma ili zionekane zimetokea nchini Zambia.

Alisema kuna uhalifu wa ukataji wa magogo ambao unafanywa na baadhi ya watu kwa ajili kuharibu maliasili ya nchini.
 
Dk. Meru alisema vyombo vya upelelezi vya wizara hiyo,  vilipata taarifa ya kuwepo na magogo bandarini ambayo yalitakiwa kusafirishwa nje ya nchi.

Alisema mara baada ya kupata taarifa hizo, walizifanyia kazi na kufanikiwa kuzikamata kontena 31 ambazo hazikuwa na kibali cha usafirishaji.

"Baada ya kuzikamata tulichokifanya tulienda kuonana na balozi wa Zambia tukawaeleza na wenyewe wanasema hawawezi kutoa kibali kwa kuwa wanakataza ukataji wa magogo nchini kwao, " alisema.

Aliongezea kuwa ; "Inawezekana magogo hayo wameyakata nchini na kufanya udanganyifu wa kwenda kuzunguka katika mpaka wa Tunduma kuonyesha kuwa yametokea Zambia, lakini balozi ameahidi kushirikiana na sisi."
  
Dk. Meru alionya yoyote atakaye bainika kuhusika katika suala hilo atachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria ili na wengine wajifunze kupitia tukio hilo.

Alisema Serikali ya Zambia na Tanzania zimeingia makubaliano ya kudhibiti biashara haramu ya ukataji wa magogo.

Naibu Balozi wa Zambia, Elizabeth Phiri, alisema sheria inazuia usafirishaji wa magogo, hivyo hana uhakika kama ni kweli vibali vimetolewa nchini kwake. Tunasubiria tupatiwe document (nyaraka) zinazoonyesha tumeruhusu usafirishaji wa magogo hayo ndipo tutalitolea taarifa, alisema Phiri
 
Naye Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala za Huduma za Misitu, Zawadi Mbwambo, alisema jumla ya kontena 37 zilizokamatwa zikiwa na magogo hayo na nyingine zipo kwenye vituo vyao vya ukaguzi.

Alisema hakuna uhakika kama kontena hizo zimesafirishwa kihalali kwa kuwa walipewa taarifa kuwa  yalikuwa yanapelekwa China kwa ajili ya kutengeneza samani na dawa.

Aidha, alisema kampuni tatu zimeonekana kuagiza mzigo huo ambazo ni Pan Atlantic, Best Ocean Air na Dar Global.

0 comments:

Post a Comment