Friday 22 July 2016

#YALIYOJIRI>>>>Tanzania Yatahadharishwa kuongezeka deni la taifa.Fahamu zaidi hapa.

Tanzania imeshauriwa kuongeza vyanzo vipya vya mapato ya ndani kwa ajili ya maendeleo na kuchukua hatua kali dhidi ya fedha haramu badala ya kutegemea mikopo ya nje.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika utambulisho wa ripoti kuhusu Maendeleo ya Uchumi barani Afrika ya mwaka 2016 ya Shirika la Maendeleo ya Biashara la Umoja wa Mataifa (UNCTAD), Claudia Roethlisberger alisema mikopo siyo njia endelevu ya maendeleo.

Alisema licha ya ripoti hiyo kuonyesha kuwa madeni ya nchi za Afrika yanahimilika, lakini Serikali za nchi za bara hilo zinatakiwa kuchukua hatua ya kuzuia ukuaji wa haraka kwa madeni ili yasiwe mgogoro kama ilivyotokea miaka ya mwishoni mwa 1980 na 1990.

Akizungumzia ripoti hiyo, mchumi kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), Prosper Charle alisema mikopo yenye masharti nafuu ambayo  Tanzania imekuwa ikitegemea imepungua na kubaki yenye masharti magumu, hivyo inapaswa kutafuta njia mbadala.

“Deni la Taifa kwa sasa linahimilika kwa sababu Tanzania ilikuwa ikipata mikopo yenye masharti nafuu ,” alisema.

Steven Mwombela kutoka Taasisi ya Utafiti wa Sera za kuondoa Umasikini (Repoa), alisema suluhisho kwa Tanzania ni kuwekeza kwenye ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi ili kupata maendeleo endelevu.

0 comments:

Post a Comment