NA HAMZA TEMBA - WMU
Waziri
 wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe ametangaza mabadiliko 
makubwa katika biashara ya mkaa nchini na kusema kuwa kuanzia mwezi 
Julai mwaka huu hakuna mkaa wowote utakaosafirishwa kutoka wilaya moja 
kwenda nyingine ili kunusuru misitu inayoteketea kwa kasi hapa nchini.
Amesema
 hayo jana  wakati akifungua mkutano wa 24 wa baraza la wafanyakazi wa 
Wizara ya Maliasili na Utalii uliofanyika katika ukumbi wa LAPF mjini 
Dodoma na kuhudhuriwa na wajumbe mbalimbali kutoka kwenye Idara, Vitengo
 na Taasisi mbalimbali zilizopo chini ya Wizara hiyo.
“Kuanzia
 mwezi Julai hakuna ruhusa ya kutoa vibali vya kuhamisha mkaa kutoka 
wilaya moja kwenda wilaya nyingine, mkaa utachomwa, utauzwa ndani ya 
wilaya kwa ajili ya matumizi ya watanzania wanaohitaji nishati ya mkaa, 
lakini biashara ya mkaa ya kutoa Dodoma kwenda Dar es Salaam mpaka 
Zanzibar marufuku.
“Wamekata
 misitu yetu yote, mito yetu imekauka, tunashindwa kupata maji ya 
umwagiliaji kwasababu watu wengi huko nje wanataka mkaa wetu, Tanzania 
jamani sio shamba la bibi, wale wote watakaotoa mkaa kutoka eneo moja 
hadi jingine kinyume na sheria hii watashuulikiwa kwa utaratibu wa 
uhujumu uchumi”, alisema Maghembe.
Alisema
 kuwa kwa upande wa miji mikubwa kama Dar es Salaam, Dodoma, Morogoro na
 Tanga vitaanzishwa viwanda maalumu vya kuzalisha mkaa ambao utauzwa kwa
 vibali maalumu katika mikoa mbalimbali hapa nchini. Amesema mkaa huo 
hautakuwa na athari nyingi za kimazingira kwa sababu utazingatia 
taratibu za uzalishaji endelevu.
Wakati
 huo huo, Waziri Maghembe amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma 
za Misitu Tanzania kumuhamisha kituo cha kazi Mkuu wa Kikosi cha 
Kufuatilia na Kuzuia Uharibifu wa Misitu wa Wakala hiyo, Arjason Mloge 
kutoka Makao Makuu ya Taasisi hiyo kwenda chuo cha Viwanda vya Misitu 
(FITI) kilichopo mkoani Kilimanjaro na badala yake atafutwe mtu mwingine
 muaminifu.
Alisema
 uamuzi huo ni kufuatia udhaifu uliojitokeza katika usafirishaji wa 
rasilimali za misitu ndani na nje ya nchi ikiwemo usafirishaji kwa 
kutumia nakala za vibali ambazo sio halisi, yaani “Photocopies”. 
“Agizo hili litekelezwe mara moja kabla ya saa sita mchana wa leo na niwe nimepewa nakala ya barua hiyo ya uhamisho” alisema.
Kufuatia
 uamuzi huo amepiga marufuku kuanzia sasa usafirishaji wa mazao ya 
misitu ndani na nje ya nchi kwa kutumia nakala zisizo halisi 
(Photocopies). Ameongeza kuwa katika kuunga mkono Sera ya Uchumi wa 
Viwanda ya Serikali ya awamu ya tano hakuna gogo litakalosafirishwa 
kwenda nje ya nchi.
“Wawekezaji
 wanahimizwa kujenga viwanda vya kuchakata magogo hayo hapa nchini ili 
kutoa ajira kwa Watanzania pamoja na kutoa faida halisi inayotokana na 
rasilimali hizo kwenye uchumi wa taifa”, alisema.
Akizungumzia
 changamoto ya mifugo kwenye maeneo ya hifadhi nchini amesema Sheria ya 
Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 sehemu ya 21 (1) hairuhusiwi
 kabisha kuchunga mifugo katika Hifadhi za Taifa, Mapori ya Akiba, 
Mapori Tengefu na Hifadhi za Misitu. Aliwataka watumishi wa Maliasili 
kusimamia Sheria hiyo pamoja na kutoa wito kwa wananchi kuifuata 
kikamilifu.
Katika
 hatua nyingine, Waziri Maghembe aliwataka majangili wote nchini 
kuachana na biashara hiyo haramu ambayo hailipi kwa sasa na badala yake 
wachukue matrekta wakalime.
“Mtu
 ambaye alikuwa anaishi kwa kutegemea ujangili sasa atafute trekta 
akalime, kwa sababu akifanya ujangili tukamkamata tu, na tukimkamata 
atakaa kwenye hoteli ya mkuu wa magereza (magereza) kwa zaidi ya miaka 
25”.
Aidha,
 Waziri Maghembe alitoa pongezi kwa watumishi wote wa Wizara ya 
Maliasili kwa kazi nzuri wanayofanya ya kupambana na ujangili nchini 
pamoja na ulinzi wa maliasili za taifa (Misitu, Wanyamapori na Mambo ya 
Kale) ambazo kwa pamoja zinachangia asilimia 20.5 kwenye pato la taifa. 
Amesema matokeo chanya ya kupambana na ujangili yameanza kuonekana japo 
ujangili bado upo.
Kwa
 upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Aloyce Nzuki 
alimueleza Waziri Maghembe kuwa maelekezo yote aliyoyatoa yamepokelewa 
kwa ajili ya kuyafanyiwa kazi, huku Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya 
Wanyamapori, Prof. Alexandre Songorwa akimueleza Waziri huyo kuwa 
watalinda na kusimamia Malisili za Taifa na kwamba katu hawapo tayari 
kuandikwa kwenye vitabu kuwa walishiriki katika kutoweka kwa maliasili 
hizo.
Download Application ya Hebron Malele Blog Kwenye Simu yako Kusoma Habari Zetu Kwa Urahisi>>>>Bonyeza Hapa
Follow me instagram>>>Bonyeza Hapa
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment