[Sehemu
 ya 3 ya Hotuba ya ndugu Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto (MB) kuhusu Mapitio 
na mwelekeo wa kazi za Serikali na Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu Kwa 
mwaka 2017/18]
Mheshimiwa Spika
Kuna
 kijana wa kitanzania, ndugu Ben Saanane amepotea kwa zaidi ya miezi 
mitano sasa. Hajulikani alipo. Wazazi wake na rafiki zake wamemtafuta na
 kutoa malalamiko bila mafanikio. Wamefikisha taarifa kwa jeshi la 
polisi na wamepaza sauti bila kuchoka. Kuna nyakati suala hili 
lilionekana la siasa na ndio maana wengine tulikaa pembeni. Lakini sasa 
ni miezi 6, kuna taarifa juu ya suala hili, nimeona nisikae kimya juu ya
 hili.
Taarifa
 zinatoka chini chini, sio rasmi, kwamba huyu kijana 'ametoweshwa'. 
Kwamba alishikiliwa na watu wa Idara ya Usalama na amepotezwa. Jeshi la 
Polisi wana taarifa za mawasiliano ya mwisho ya Ben Saanane kwa kutumia 
simu yake ya mkononi, ambayo inaonekana simu ilipoteza mawasiliano akiwa
 maeneo ya Buguruni siku aliyotekwa tarehe 15/16 Novemba 2016 na tangu 
siku hiyo hapakuwa na mawasiliano tena.
Siku
 hiyo simu yake ilisoma maeneo ya Tabata asubuhi, kisha Mikocheni na 
Mwenge muda mwingi wa mchana. Saa mbili usiku alikuwa Mburahati na saa 
nne usiku ilizimwa akiwa Buguruni. Polisi wanajua kuwa wenzao wa Usalama
 wa Taifa ndio waliomteka kijana huyu lakini hawawezi kuchukua hatua 
dhidi yao. Hivyo wameamua kukaa kimya wakiamini kuwa Watanzania 
tutasahau.
Jambo
 hili linasikitisha na kuumiza sana, Ben ni kijana wa kitanzania, ni 
mtoto, mjomba, baba, kaka, anayo familia, siwezi hata kufikiria ni namna
 gani familia yake inaumia kwa miezi hii sita bila kumuona ndugu yao, 
bila kujua alipo, bila kujua hatma yake. Inaumiza sana, inaumiza mno, ni
 jambo gumu sana kulivumilia, si jambo rahisi kulipuuzia na kusahau tu. 
Watanzania hatupaswi kukalia kimya kuhusu jambo hili, tukisahau hili 
hakuna atakayepona.
Kumekuwa
 na matukio ya namna hii mabaya kabisa huko nyuma; ndugu Absalom 
Kibanda, aliyekuwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri alivamiwa na 
kuumizwa vibaya sana na leo jicho lake moja halioni mwaka 2013. Pia 
ndugu Yona wa Temeke alitekwa na kuumizwa na kutupwa huko mbweni jijini 
Dar es salaam na hakuna mtu yeyote aliyekamatwa juu ya matukio yote 
hayo. Orodha ya matukio ya namna hii ni ndefu.
Watanzania
 wamesahaulishwa yote haya, Polisi mpaka Leo hawajamkamata hata mtu 
mmoja juu ya yote hayo. Sababu kubwa ni ukimya wetu. Sisi wabunge 
tumepewa ridhaa na wananchi wenzetu kuyasema haya, tumepewa mamlaka ya 
kuihoji serikali juu ya mambo ya wananchi, na Usalama wao na mali zao ni
 jambo la kwanza la msingi kabisa, wananchi wetu wakiwa na mashaka juu 
ya usalama wao, shughuli za uzalishaji mali zitakuwa duni, uchumi wa 
Taifa utadorora zaidi. Tunao wajibu wa kuhakikisha Usalama wa wananchi 
wetu, ni wakati wa kuibana Serikali juu ya hili.
Mheshimiwa Spika,
Naomba
 kulikumbusha Bunge lako Tukufu na wananchi Kwa ujumla kwamba Usalama wa
 Taifa hawana mamlaka yeyote kisheria kukamata mtu yeyote yule Kwa 
mujibu wa kifungu cha 5(2) cha sheria ya usalama wa Taifa ya mwaka 1996 
Kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kadhaa. Kwa hiyo Askari wa Usalama 
wa Taifa waliokwenda Clouds Media na silaha, Askari wa Usalama 
aliyemtolea silaha Mbunge wa Mtama, ndugu Nape, na kikosi cha utekaji na
 utesaji cha Usalama wa Taifa kinachohusishwa na utekaji wa watu 
wanavunja sheria ya usalama wa Taifa.
Hata
 askari wa Usalama wa Taifa waliomkamata Mbunge wa Geita Vijijini, ndugu
 Msukuma, Mbunge wa Nzega, ndugu Bashe na Mbunge mstaafu, ndugu Malima 
walivunja sheria ya Usalama wa Taifa. Kuna viashiria vyote kuwa hali si 
nzuri kabisa.
Lakini
 kuna jambo moja muhimu sana juu ya jambo hili, MTAZAMO HASI wa 
Watanzania juu ya Idara ya Usalama wa Taifa. Idara Nyeti, Muhimu na ya 
Kuheshimiwa mno kwa Taifa letu, inaniuma leo kusimama hapa Bungeni 
kuisema Idara ya Usalama wa Taifa. Mimi niko Bungeni mwaka wa 12 huu, 
hatuzungumzii mambo ya Usalama wa Taifa humu bungeni, jambo hilo ni 
'Taboo', lakini kwa hali ilivyo sasa imenibidi niseme.
Mambo
 haya maovu yanayohusishwa na Idara hii yanaondoa uhalali wa Taasisi hii
 kwa wananchi, yanaondoa heshima, hadhi na uaminifu juu ya idara hii, 
yanajenga chuki na taswira hasi ya Wananchi kwa idara hii, hili si jambo
 jema kwa Taifa. Ni wakati sasa wa kuchukua hatua. Ni lazima Bunge 
liamke na kukomesha hali hii.
Kwa
 mujibu wa Kanuni ya 120(2) ya Kanuni za Bunge natoa Taarifa kwamba 
nitatoa hoja binafsi kutaka Bunge lako Tukufu kuunda Kamati Teule 
kufanya uchunguzi kuhusu vitendo vya utekaji, uteswaji na hata mauaji 
dhidi ya raia (suala la Ben Saanane likiwemo).
Pamoja
 na mambo mengine, Kamati teule hiyo pia nitapendekeza iangalie namna ya
 kufanya mabadiliko makubwa kwa Idara ya Usalama wa Taifa ili kuiondoa 
kuwa Idara ya utesaji na badala yake kuwa idara ya kulinda Wananchi, 
Rasilimali za nchi na Ulinzi wa Katiba ya nchi.
Naamini wabunge wenzangu mtaniunga mkono kwenye hili.
Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Mbunge - Kigoma Mjini (ACT Wazalendo)
Dodoma
Aprili 11, 2017
Download Application ya Hebron Malele Blog Kwenye Simu yako Kusoma Habari Zetu Kwa Urahisi>>>>Bonyeza Hapa
Follow me instagram>>>Bonyeza Hapa
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment