Hatimaye Jeshi la Polisi 
limetoa kibali cha kufanya mkutano wa hadhara kwa Mbunge wa Iringa 
Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, lakini limeweka mlolongo wa masharti 
ambayo atalazimika kuyatii kuepuka rabsha.
Wakati Jeshi la Polisi 
likitoa masharti hayo, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu amesema 
vyama vya upinzani vitaendelea kuendesha mikutano ya hadhara licha ya 
kufungua kesi Mahakama Kuu ya kupinga zuio la shughuli hizo, huku 
akisema amri ya kuzuia wanasiasa kufanya mikutano nje ya maeneo yao 
imetolewa bila ya kusoma sheria. 
Mkoani Iringa, Jeshi la Polisi lilitoa masharti hayo baada ya Msigwa, ambaye anaongoza Jimbo la Iringa 
Mjini kwa kipindi cha pili mfululizo, kutaarifu kuwa atafanya mkutano wa
 hadhara kuanzia Septemba Mosi, siku ambayo Chadema imepanga kuanza 
operesheni ya nchi nzima inayoiita “ya kupinga udiktekta Tanzania”. 
Katika barua aliyomwandikia Mchungaji Msigwa juzi, Mkuu wa Polisi wa 
Wilaya ya Iringa (OCD), Y. Z Mjengi amerejea barua ya mbunge huyo yenye 
kumbukumbu namba MB/IR/M/05 ya Agosti Mosi mwaka huu, inayohusu mikutano
 ya hadhara kuanzia Agosti 3 hadi 22, ikianza saa 8:00 mchana hadi 12:00
 jioni. 
Kupitia barua hiyo, ambayo Msigwa alithibitisha kuipokea, Jeshi 
la Polisi limesema limeridhia kwa sababu lengo la mkutano wake ni 
kuhamasisha maendeleo na kupokea kero za wananchi, kazi ambayo inatakiwa
 kufanywa na mbunge wa eneo husika.
“Natarajia mkutano wako (Msigwa) 
utakuwa wa amani na utulivu bila kumkashifu mtu wa chama kingine,” 
anasema Mjengi katika barua hiyo. 
“Mikutano yote hiyo kibali kimetolewa kwako kama mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini. Sitarajii
 mtu mwingine kutoka nje ya Mkoa wa Iringa kuja kukusemea kuhusu 
maendeleo ya jimbo lako au kuja kupokea kero za wananchi wako na 
kuzijibia wakati hiyo ni kazi ya mwenye himaya ambaye ni wewe. 
“Kashfa, 
kejeli, matusi na maneno ya uchochezi kwa viongozi wa Serikali 
vitahesabiwa ni uvunjifu wa amani na hatua kali za kisheria 
zitachukuliwa dhidi yako na zitapelekea kuzuiliwa kufanya mikutano yako 
inayoendelea.” 
Barua hiyo inaishia kwa maneno yaliyoandikwa kwa herufi 
kubwa. “Kumbuka: Amani ya Tanzania italindwa na kila Mtanzania kwa hiyo 
ni jukumu lako wewe Mhe. Mbunge kutekeleza jukumu la ulinzi wa amani. 
Kwa pamoja tutaweza,” inasema barua hiyo. 














0 comments:
Post a Comment