Madudu
 mengine yameibuliwa katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia baada 
ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serilali (PAC) kupitia taarifa za 
Manunuzi na za kihasibu za wizara hiyo wakati sakata la wanafunzi hewa 
likiendelea kufukuta.
Kamati
 hiyo imebaini kuwa shilingi bilioni 1.2 zilitumika kwa ajili ya kuandaa
 hafla ya harambee ya Wizara hiyo nchini Marekani, tukio ambalo hata 
hivyo halikufanyika.
Kwa
 mujibu wa maelezo ya wizara hiyo, harambee hiyo ilitarajiwa kukusanya 
zaidi ya dola milioni 3 za Marekani ambazo ni sawa na shilingi bilioni 6
 za Kitanzania.
Wajumbe
 wa PAC walihoji matumizi ya fedha hizo. Hivyo, Gerald Mwaja ambaye 
anahusika na mipango alilazimika kutoa majibu ambayo hata hivyo 
yalionekana kutowaridhisha wajumbe wa Kamati hiyo.
Alisema
 kuwa fedha hizo zilitumika kwa ajili ya mradi huo ambao ulikuwa na 
malengo matatu, kati ya malengo hayo lengo moja la kufanya harambee hiyo
 lilishindwa lakini malengo mengine mawili yalifanikiwa.
“Mradi
 wenyewe ulikuwa na malengo matatu; kuongeza matumizi ya teknolojia ya 
Mawasiliano, kuja na mbinu za kufundishia na pia kukusanya fedha kwa 
awamu,” alisema.
Alisema malengo mawili yaliyotimia ni kuongeza matumizi ya teknolojia ya mawasiliano pamoja na mbinu ya kufundishia.
Katika
 hatua nyingine, PAC imebaini kuwa Wizara hiyo ilitenga kiasi cha 
shilingi bilioni 2.1 na kuingia mkataba na Kampuni ya Ujenzi ya Magereza
 mwaka 2014 kwa ajili ya kujenga jengo la ghorofa tatu la ofisi za 
wizara hiyo Mkoani Dodoma lakini jengo hilo halijajengwa hadi sasa.
Mbunge
 wa Vwawa (CCM), Josephat Asunga alisema kuwa wamebaini kuwa sheria ya 
manunuzi ya umma haikufuatwa na kwamba mkandarasi alilipwa kiasi 
shilingi milioni 780.6 kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo hata kabla ya 
mkataba kusainiwa.
Aliongeza
 kuwa hakukuwa na maelezo yoyote yanayoonesha kulikuwa na mshindani 
katika zabuni hiyo huku fedha nazo zikilipwa kwenye akaunti ya mtu 
aliyetajwa kwa jina la Mang’ula badala ya akaunti ya kampuni ya 
Magereza.
Pia,
 Asunga alieleza kuwa kabla ya ujenzi kuanza mwaka 2015, Wizara hiyo 
ilibadili mpango wa kujenga jengo hilo kwa ghorofa tatu na kuwa jengo la
 ghorofa nne litakalogharimu shilingi bilioni 4.4.
“Baada
 ya Rais Magufuli kuagiza kuwa wote tunahamia Dodoma, wamebadilika 
wanasema hawajapata eneo la ujenzi wakati walishasema awali wamepata 
eneo,” alisema Asunga.
Aliyekuwa
 waziri wa Waziri wa Elimu wakati huo, alieleza kuwa hakufahamishwa 
lolote kuhusu ujenzi wa jengo hilo na kwamba hata muhtasari wa mpango 
huo hakupewa kwa ajili ya kushauri.
“Mimi
 kama Waziri sikujua kinachoendelea katika ujenzi wa jengo, na hata 
briefing (muhtasari) ilikosekana ili niweze kushauri,” alisema.
Akijibu
 maswali hayo, Afisa Manunuzi wa Wizara hiyo, Audifasy Myonga alikiri 
kuwa utaratibu wa manunuzi haukufuatwa na kwamba kulipaswa kuwa na 
mshauri mwelekezi ili kutimiza matakwa ya Sheria.
Kaimu
 Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Hillary Aeshi aliagiza kupitiwa upya kwa 
mchakato wa zabuni ya Jengo la ofisi ya wizara hiyo mjini Dodoma na 
kuwasilisha taarifa ya utekelezaji kwenye ofisi ya Katibu wa Bunge kabla
 ya Septemba Mosi mwaka huu.
 









 




 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment