Friday 30 October 2015

#MICHEZO>>>Azam yakwaa kileleni ligi kuu Vodacom Tanzania Bara baada ya kuendeleza ushindi.Fahamu zaidi hapa.

TIMU ya Azam FC yaonesha nia ya kuchukua kombe la ligi kuu Vodacom Tanzania Bara baada ya kuendeleza mfululizo wa kushinda michezo yake ya ligi kuu Vodacom Tanzania Bara imekaa kileleni kwa mara ya kwanza msimu huu baada ya kuichapa JKT Ruvu mabao 4-2 kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania uliofanyika Uwanja wa Karume jioni ya leo.

Azam FC inakaa kileleni baada ya kufikisha jumla ya pointi 22 na kuishusha Yanga yenye pointi 20 baada ya jana kuambulia sare ya mabao 2-2 dhidi ya Mwadui.
Kocha wa Azam FC, Stewart Hall, alifanya marekebisho kwenye eneo la ushambuliaji la timu yake katika mchezo wa leo, akimuanzisha kwa mara ya kwanza mshambuliaji Didier Kavumbagu raia wa Burundi.

Kavumbagu aliitumia vema nafasi hiyo aliyopewa baada ya kuifungia bao la uongozi Azam FC katika dakika ya 4 akitumia vema pasi safi ya Michael Bolou na kupiga shuti la kiufundi lililomshinda kipa wa JKT, Shabani Dihile.

Dakika mbili baadaye nahodha wa Azam FC, John Bocco, aliitumia vema krosi safi ya beki wa kulia Shomari Kapombe na kupiga shuti safi lililomshinda kipa wa JKT.

Winga msumbufu wa JKT Ruvu, Najim Magulu, aliipatia timu yake bao la kwanza dakika ya 31 kwa shuti akiwa ndani ya eneo la 18 akiunasa mpira wa adhabu ndogo uliopigwa na mshambuliaji Saady Kipanga na kuwababatiza mabeki wa Azam FC.

Hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika, Azam iliondoka kifua mbele kwa mabao 2-1, ambapo kipindi cha pili kilianza kwa Hall kumtoa kiungo Michael Bolou na kuingia Himid Mao, JKT Ruvu nayo ilimtoa mshambuliaji Gaudence Mwaikimba na kuingia Samwel Kamuntu.

Mwamuzi wa mchezo wa leo, Israel Nkongo kutoka Dar es Salaam aliamuru penalti ipigwe langoni mwa JKT Ruvu dakika ya 63 baada ya beki wa timu hiyo Paul Mhidze, kumkwatua beki wa Azam FC, Shomari Kapombe.

Bocco aliihakikishia Azam FC ushindi kwa kufunga vema penalti hiyo dakika ya 64 kwa kuandika bao la tatu kwa timu na la tatu kwake msimu huu kwenye ligi hiyo, JKT Ruvu ilirejea mchezoni baada ya kupata bao la pili dakika 69 lililofungwa na Emmanuel Pius.

Hall alifanya tena mabadiliko dakika ya 77 kwa kumtoa Bocco na kuingia Kipre Tchetche, ambaye aliifungia bao la nne Azam FC dakika ya 90 akipiga shuti la kiufundi la juu baada ya kuwahadaa mabeki wa JKT Ruvu pembeni ya uwanja na kupiga shuti hilo lililomshinda kipa wa JKT.

0 comments:

Post a Comment